PSSSF IMETOA ELIMU YA HUDUMA NA UWEKEZAJI KWA WABUNGE
Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF), Aprili 03,2025 umetoa elimu ya shughuli za Uwekezaji na Huduma zinazotolewa na PSSSF kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji naMitaji ya Umma (PIC)
Akizungumza katika ufunguzi wa Mafunzo hayo Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko Bw. Abdul-Razaq Badru ameiambia kamati hiyo kuwa shughuli kuu za Mfuko ni Usajili, Ukusanyaji wa michango, uwekezaji na ulipaji wa maafao kwa wanachama.Aidha, ameiambia kamati kuwa Mfuko unawekeza ili kuzalisha kiwango kilichochangiwa na mwanachama ili anapostaafu aweze kulipwa zaidi kutoka na mabadiliko ya kiuchumi na kuongeza kuwa Mfuko unawekeza kwa kuangalia ustahimilivu wa Mfuko miaka 50 mbele.
Katika kikao hicho, PSSSF ilieleza ilivyowekeza katika sekta mbalimbali, ikiwemo ujenzi wa nyumba, masoko ya hisa, viwanda na majengo ya ofisi.
Waheshimiwa wabunge wameipongeza PSSSF kwa juhudi kubwa katika kutoa huduma za kisasa, kitaalamu na zenye ubunifu mkubwa, ambazo zinasaidia katika kuwahudumia wanachama kwa wakati na kupunguza malalamiko.
Wabunge hao walitoa wito kwa PSSSF kuendelea na juhudi za kutoa elimu kwa wanachama na wastaafu ili kuwajengea uelewa mzuri kuhusu matumizi ya fedha zao katika uwekezaji ili kuongeza uwazi na kuimarisha uhusiano kati ya PSSSF na wanachama wake.
Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mh. Augustine Vuma Holle ameipongeza PSSSF kwa ubunifu na utaalam katika kuwahudumia wanachama na wastaafu na kuwaomba PSSSF kuendelea kuwekeza kwenye maeneo yenye tija ili kuleta tija kwa Jamii na taifa kwa ujumla